Skip to main content

BARAZA LA WAFANYAKAZI OFISI YA MWANASHERIA MKUU LAKUTANA

 






Mwanasheria Mkuu wa Serikali asisitiza kuendelea kusogeza huduma karibu na Wananchi

Baraza la Wafanyakazi la Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali limekutana na kufanya kikao kwa ajili ya kujadili masuala mbalimbali yatakayosaidia kurahisisha utendaji kazi na kutoa huduma bora zaidi za kisheria kwa wananchi. 

Kikao hicho kimefanyika Januari 24, 2025 katika Chuo cha Uongozi cha Mwalimu Nyerere kilichopo Kibaha Mkoani, Pwani kwa kuwashirikisha wajumbe kutoka Divisheni, Vitengo na wajumbe wa TUGHE kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali. 

Akizungumza wakati wa kikao cha Baraza hilo, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe, Hamza S. Johari, amesema kuwa lengo la kikao hicho ni kufanya tathmini ya utendaji kazi wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na kujadili na kuzipatia ufumbuzi changamoto mbalimbali ili kuleta ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya Ofisi.

“Tumekutana kwenye kikao hiki cha Baraza na kupitia kwa pamoja changamoto zetu hasa suala la mafunzo kwa Mawakili wetu, wapate mafunzo katika kiwango kinachohitajika, na namna tunavyoweza kutumia TEHAMA hususan mfumo wetu wa OAG - MIS katika kuboresha utoaji wa huduma zetu.” amesema Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Aidha, Mwanasheria Mkuu wa Serikali amesema kuwa ni wazi kuwa mwaka uliopita Ofisi ya Mwanasheri Mkuu wa Serikali wamefanya vizuri katika eneo la utoaji wa huduma za ushauri wa kisheria ikiwemo uanzishwaji wa Kliniki za Ushauri wa Kisheria ambazo zimeendelea kutolewa bure kwa wananchi katika maeneo mbalimbali nchini.

“Kwa mwaka uliopita tumeweza kuanzisha Kliniki za Kisheria tukiwa na lengo la kusogeza huduma za kisheria kwa wananchi katika maeneo yao wanayoishi, na hivi sasa huduma hii tunaendelea kuitoa kwa wananchi wa mkoa wa Kilimanjaro”. Amesema Mhe. Johari 

Kwa upande wake Mgeni Rasmi katika ufunguzi wa kikao cha Baraza la Wafanyakazi la Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Bw. Eliakim Maswi, ameipongeza ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa namna ambavyo wamekuwa wakitekeleza majukumu yao, sambamba na kuitisha kikao cha Baraza la Wafanyakazi kujadili masuala mbalimbali yanayohusu ofisi hiyo. 

Katika hatua nyingine Bw. Maswi ametoa wito kwa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuendelea kutoa mafunzo kuhusu Upekuzi wa Mikataba kwa Mawakili wa Serikali ili kuhakikisha wanaendelea kusimamia vizuri mikataba ya Serikali kwa maslahi mapana ya Taifa. 

“Wito wangu kwa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, ni kuendelea kutoa mafunzo ya upekuzi wa Mikataba kwa Mawakili wa Serikali ili kuendelea kuboresha utendaji kazi wa Mawakili na Wanasheria wetu katika kusimamia Mikataba mbalimbali ambayo ina maslahi mapana kwa nchi.” Amesema Bw. Maswi.

Awali akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao hicho, Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Samwel Maneno, amesema katika kipindi cha mwaka 2024/2025 Jumla ya mikataba 1,799 ilifanyiwa upekuzi ambapo kati ya hiyo mikataba 1,639 ya manunuzi,120 imehusu fedha,mkataba (1) kuhusu Maliasili na 39 ni ya ushirikiano wa Kimataifa.

Nae Mwenyekiti wa TUGHE tawi la Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Bi. Zella Rwemanyira Ametoa rai kwa watumishi wa ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuendelea kufanya kazi kwa bidii ili waweze kuendana na dhana ya Weledi na Ubora.

“Natoa rai kwa Watumishi wenzangu wa Ofisi ya Mwanasheria kuendelea kuchapa kazi kwa bidi ili tuendane na dhana ya Weledi na Ubora.” Amesema Bi. Zella.

Comments

Popular posts from this blog

MWAKIPOSA MWENYEKITI MPYA WA WENYEVITI WA SERIKALI ZA MITAA DAR

Mwenyekiti wa Serikali ya mtaa wa Boko Wilaya ya Kinondoni, Razalous Mwakiposa ameibuka mshindi wa nafasi ya Mwenyekiti wa wenyeviti wa Serikali za mitaa mkoa wa Dar es Salaam kwa kupata kura 24 kati ya 37 zilizopigwa na wajumbe mapema leo hii. Uchaguzi huo umemalizika leo June 20, 2026ambapo  ulikua unahusisha nafasi ya Mwenyekiti na Katibu Mkuu, ambapo Mwenyekiti ameshinda Razalous Mwakiposa huku Katibu Mkuu akiwa ni Peppino Sudi Peppino . Akizungumza wakati wa kutangaza matokeo ya uchaguzi huo, msimamizi wa uchaguzi, Kambi Sinde, amesema kuwa Razalous Mwakiposa ameshinda kwa kupata kura 24 kati ya kura 37 zilizopigwa, huku Katibu Mkuu akishinda kwa kura 20 kati ya kura 37 zilizopigwa. "Uchaguzi umefanyika kwa uwazi na haki, kulikuwa na jumla ya wajumbe 40, lakini watatu walipata udhuru, hivyo, leo waliopiga kura ni wajumbe 37 na matokeo ni kwamba mshindi wa nafasi ya Mwenyekiti amepata kura 24 kati ya kura 37 zilizopigwa, huku Katibu Mkuu akipata kura 20 kati ya kura 37 zilizop...

TIRDO YAVUNJA VIKWAZO VYA UBUNIFU, AFRO HEAL YAGEUZA MIMEA YA ASILI KUWA DAWA ZA KISASA

Na Ayra News.  Mashauri Enock Shushu, kutoka Afro heal Group Limited, amesema malezi ya ubunifu kupitia shirika la Utafiti na Maendeleo ya Viwanda Tanzania (TIRDO) yameiwezeshaa kampuni hiyo kubadili dawa za asili zilizokuwa zikitengenezwa kwa kutumia magome ya miti na kuzigeuza kuwa bidhaa za kisasa zinazokidhi viwango vya ubora na mahitaji utengenezaji soko. Akizungumza katika Maonesho ya Nanenane 2026, Shushu alisema Afro healGroup Limited ni kampuni inayojihusisha na utafiti na utengenezaji wa dawa za binadamu zinazotokana na mimea ya asili, huku TIRDO ikiwa imekuwa nguzo muhimu katika kukuza uwezo wao wa ubunifu na uzalishaji. Alisema kabla ya kujiunga na TIRDO, kampuni hiyo ilikuwa ikitengeneza dawa za asili katika mfumo wa magome, lakini baada ya kupata malezi ya biashara, ushauri wa kitaalamu na uwekezaji wa rasilimali watu kupitia taasisi hiyo, imefanikiwa kuziboresha na kuzalisha bidhaa za kisasa zinazorahisisha matumizi kwa wananchi. Shushu alisema ushirikiano kati ya wa...

VETA KAGERA WABUNI MTEGO KISASA WA KUVUNA SENENE

Ayra Nwestz  Chuo cha Veta mkoa wa Kagera VTC kimebuni mtambo wa kisasa wa kuvuna senene ambao unamuwezesha mvunaji kunapata senene wengi kwa wakati mmoja ambao wanakua salama. Akizungumza na Mtandao wa Matukio Daima, katika maonyesho ya 47 ya biashara ya kimataifa, Mwalimu wa Kagera VTC, Elias Lucas Mayala, amesema chuo hicho kimebuni mtego huo una lengo la kupunguza uharibifu wa mazingira unaotokana na mbinu za jadi za uvunaji. Mayala amesema kuwa mtanbo huo una uwezo wa kubeba kati ya kilo 80 hadi 100 za senene kwa wakati mmoja wakati wa uvunaji.  Aidha, amesema mtego huo una mfumo wa kuchuja senene wanapoingia na kuwatenganisha wadudu wadogo wadogo, ambao wanaweza kutumika kama chakula cha kuku badala ya kutupwa. Ameeleza kuwa tofauti na mbinu za zamani zinazoweza kuharibu miti na mazalia ya senene, mtego huo ni rafiki wa mazingira na umeundwa kwa namna inayorahisisha matumizi yake, ikiwa ni pamoja na uwezo wa kusogezwa kutoka eneo moja kwenda jingine kulingana na mahitaji...