Skip to main content

BENKI YA EQUITY NA SERIKALI KUIMARISHA SEKTA YA MIFUGO NA NGOZI NCHINI

 







Dodoma – 24 Julai 2025

Benki ya Equity kwa kushirikiana na Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeanzisha mpango mahsusi wa kuimarisha sekta ya Mifugo na Ngozi nchini, kwa lengo la kuongeza thamani ya mazao ya Mifugo, kupanua masoko na kuinua maisha ya wafugaji.

Akizungumza katika kikao cha wadau wa sekta ya mifugo, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dk. Edwin Mhede, alisema serikali imeitaka Benki ya Equity na Bodi yake kushirikiana na serikali kuunda timu maalum ya kitaalamu itakayosimamia uwekezaji katika sekta ya Mifugo.

“Hatua hii inalenga kuboresha ufugaji na mifumo ya uzalishaji wa ngozi, kuongeza ubora na kuifanya sekta hii kuwa chanzo kikuu cha mapato kwa wafugaji,” alisema Dk. Mhede.

Aliongeza pia ili kuboresha Sekta ya Mifugo nchini, hasa kupambana na Magonjwa, Serikali tayari inaendesha kampeni ya kuchanja mifugo yote nchini, ambapo mpaka sasa imechanja zaidi ya mifugo milioni 16, na zoezi hili linatarajiwa kukamilika ifikapo Oktoba mwaka huu, ili kuhakikisha mazao ya Mifugo ikiwemo ngozi yanakidhi viwango vya soko la ndani na kimataifa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Equity Group Holdings, Dk. James Mwangi, alisema mpango huu wa ushirikiano na uwekezaji unaendana na dira ya benki ya kuendeleza sekta muhimu za uchumi barani Afrika.

“Tunataka wafugaji wafaidike si kwa kuuza mifugo na ngozi ghafi pekee, bali kwa kushiriki kikamilifu katika minyororo mizima ya thamani. Equity Group ipo tayari kuwekeza katika teknolojia na ufadhili utakaobadilisha sekta ya Mifugo na Ngozi nchini,” alisema Dk. Mwangi.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Equity Tanzania, Bi. Isabela Maganga, alibainisha kuwa benki hiyo imejipanga kuwekeza moja kwa moja katika sekta ya Mifugo na Ngozi kwa kushirikiana na serikali na wadau wengine. Lengo ni kuwawezesha wafugaji, hasa wa vijijini, kupata masoko yenye tija na kuongeza kipato kupitia uboreshaji wa minyororo mizima ya thamani.

“Tumeandaa mikakati ya kifedha na kiufundi kwa ajili ya kuwasaidia wafugaji kupata mikopo nafuu, kushiriki katika usindikaji na kufikia masoko ya ndani na nje ya nchi,” alisema Bi Isabela Maganga.

Mwenyekiti wa Bodi ya Benki ya Equity, Bw Florens Turuka, aliongeza kuwa sekta ya Mifugo na Ngozi inatoa fursa kubwa za kiuchumi, na akawataka wafugaji kushirikiana na benki kupata mikopo na msaada wa kitaalamu ili kuinua uzalishaji na thamani ya ngozi.

Takwimu za sasa zinaonesha kuwa Tanzania ina ng’ombe takriban milioni 34, mbuzi milioni 24.5 na kondoo milioni 8.5. Sekta ya mifugo inachangia takriban asilimia 7.4 ya Pato la Taifa. 

Akiwasilisha mada katika mkutano huo, Mkurugenzi wa Biashara wa Benki ya Equity, Bw. Prosper Nambaya, alisema uwekezaji huu ni suluhisho la muda mrefu kwa changamoto ya Sekta ya Mifugo na uuzaji ngozi ghafi bila usindikaji.

“Kwa kutumia teknolojia za kisasa na kuunganisha masoko, Tanzania inaweza kuongeza ubora wa Mifugo na thamani ya ngozi zinazozalishwa mara mbili au tatu zaidi, hivyo kuongeza ajira, mapato na mchango wa sekta hii kwenye uchumi,” alisema Nambaya.

Baadhi ya wafugaji walioshiriki mkutano huo walieleza changamoto mbalimbali zinazoikabili sekta ya mifugo, zikiwemo ukosefu wa elimu ya Ufugaji wa Kisasa, uhaba wa malisho na maji, uzalishaji mdogo, miundombinu duni, ukosefu wa mitaji, bima na masoko ya uhakika. Hata hivyo, waliipongeza Benki ya Equity kwa mpango huu, wakisema unaleta matumaini mapya kwa maendeleo ya sekta hiyo.

Utekelezaji wa ushirikiano huu unatarajiwa kuongeza ajira kwa wanawake na vijana katika minyororo ya thamani ya Mifugo na Ngozi kuanzia ufugaji, ukusanyaji, usindikaji hadi masoko, sambamba na kuongeza mchango wa sekta ya mifugo kwenye pato la taifa.

Comments

Popular posts from this blog

MWAKIPOSA MWENYEKITI MPYA WA WENYEVITI WA SERIKALI ZA MITAA DAR

Mwenyekiti wa Serikali ya mtaa wa Boko Wilaya ya Kinondoni, Razalous Mwakiposa ameibuka mshindi wa nafasi ya Mwenyekiti wa wenyeviti wa Serikali za mitaa mkoa wa Dar es Salaam kwa kupata kura 24 kati ya 37 zilizopigwa na wajumbe mapema leo hii. Uchaguzi huo umemalizika leo June 20, 2026ambapo  ulikua unahusisha nafasi ya Mwenyekiti na Katibu Mkuu, ambapo Mwenyekiti ameshinda Razalous Mwakiposa huku Katibu Mkuu akiwa ni Peppino Sudi Peppino . Akizungumza wakati wa kutangaza matokeo ya uchaguzi huo, msimamizi wa uchaguzi, Kambi Sinde, amesema kuwa Razalous Mwakiposa ameshinda kwa kupata kura 24 kati ya kura 37 zilizopigwa, huku Katibu Mkuu akishinda kwa kura 20 kati ya kura 37 zilizopigwa. "Uchaguzi umefanyika kwa uwazi na haki, kulikuwa na jumla ya wajumbe 40, lakini watatu walipata udhuru, hivyo, leo waliopiga kura ni wajumbe 37 na matokeo ni kwamba mshindi wa nafasi ya Mwenyekiti amepata kura 24 kati ya kura 37 zilizopigwa, huku Katibu Mkuu akipata kura 20 kati ya kura 37 zilizop...

TIRDO YAVUNJA VIKWAZO VYA UBUNIFU, AFRO HEAL YAGEUZA MIMEA YA ASILI KUWA DAWA ZA KISASA

Na Ayra News.  Mashauri Enock Shushu, kutoka Afro heal Group Limited, amesema malezi ya ubunifu kupitia shirika la Utafiti na Maendeleo ya Viwanda Tanzania (TIRDO) yameiwezeshaa kampuni hiyo kubadili dawa za asili zilizokuwa zikitengenezwa kwa kutumia magome ya miti na kuzigeuza kuwa bidhaa za kisasa zinazokidhi viwango vya ubora na mahitaji utengenezaji soko. Akizungumza katika Maonesho ya Nanenane 2026, Shushu alisema Afro healGroup Limited ni kampuni inayojihusisha na utafiti na utengenezaji wa dawa za binadamu zinazotokana na mimea ya asili, huku TIRDO ikiwa imekuwa nguzo muhimu katika kukuza uwezo wao wa ubunifu na uzalishaji. Alisema kabla ya kujiunga na TIRDO, kampuni hiyo ilikuwa ikitengeneza dawa za asili katika mfumo wa magome, lakini baada ya kupata malezi ya biashara, ushauri wa kitaalamu na uwekezaji wa rasilimali watu kupitia taasisi hiyo, imefanikiwa kuziboresha na kuzalisha bidhaa za kisasa zinazorahisisha matumizi kwa wananchi. Shushu alisema ushirikiano kati ya wa...

VETA KAGERA WABUNI MTEGO KISASA WA KUVUNA SENENE

Ayra Nwestz  Chuo cha Veta mkoa wa Kagera VTC kimebuni mtambo wa kisasa wa kuvuna senene ambao unamuwezesha mvunaji kunapata senene wengi kwa wakati mmoja ambao wanakua salama. Akizungumza na Mtandao wa Matukio Daima, katika maonyesho ya 47 ya biashara ya kimataifa, Mwalimu wa Kagera VTC, Elias Lucas Mayala, amesema chuo hicho kimebuni mtego huo una lengo la kupunguza uharibifu wa mazingira unaotokana na mbinu za jadi za uvunaji. Mayala amesema kuwa mtanbo huo una uwezo wa kubeba kati ya kilo 80 hadi 100 za senene kwa wakati mmoja wakati wa uvunaji.  Aidha, amesema mtego huo una mfumo wa kuchuja senene wanapoingia na kuwatenganisha wadudu wadogo wadogo, ambao wanaweza kutumika kama chakula cha kuku badala ya kutupwa. Ameeleza kuwa tofauti na mbinu za zamani zinazoweza kuharibu miti na mazalia ya senene, mtego huo ni rafiki wa mazingira na umeundwa kwa namna inayorahisisha matumizi yake, ikiwa ni pamoja na uwezo wa kusogezwa kutoka eneo moja kwenda jingine kulingana na mahitaji...