Skip to main content

DOYO: AAHIDI RUZUKU MAALUM KWA WATU WENYE ULEMA­VU

 



Asema: Serikali Ya NLD Itapunguza Kodi Kwa Wawekezaji Ili Kutoa Mitungi Ya Gesi Bure Kwa Watanzania, Ni Hatua Ya Kuokoa Mazingira.

Moshi, Kilimanjaro

Akiwa katika ziara yake ya kampeni mkoani Kilimanjaro, Mgombea Urais wa Chama cha National League for Democracy (NLD), Mhe. Doyo Hassan Doyo, amewahakikishia Watanzania kwamba serikali atakayoiongoza itakuwa ya usawa, matumaini na maendeleo kwa kila Mtanzania bila ubaguzi, huku lengo lake kuu likiwa ni kuimarisha usawa wa kijamii na kiuchumi.

Mhe. Doyo amesema wazi kwamba serikali ya NLD itahakikisha makundi maalum nchini yanapewa nafasi na msaada unaostahili. Watu wenye ulemavu, wasioona, wenye ulemavu wa ngozi, na wale wenye changamoto mbalimbali za kimaumbile hawatasahaulika tena iwapo wananchi watamchagua Oktoba 29.

“Serikali yangu itatenga ruzuku maalum kwa watu wenye uhitaji maalum. Tutaanzisha mfumo mahsusi wa kuwasaidia moja kwa moja, bila urasimu, bila foleni, na bila kulazimika kupita kwenye milango ya wizara zisizo na majibu ya haraka kwa watu wenye uhitaji,” alisema Mhe. Doyo kwa msisitizo huku akishangiliwa na wananchi.

Amesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha kila Mtanzania anapata nafasi sawa ya kuishi kwa heshima, kujitegemea kiuchumi, na kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa taifa jipya lenye utu, uzalendo, haki na maendeleo.

Aidha, Mhe. Doyo amesema serikali yake itahakikisha kuwepo kwa utambulisho maalum kwa watu wenye uhitaji maalum, hasa watu wenye ulemavu, sambamba na mikakati maalum ya kitaifa ya kuwapatia makazi, afya bora, elimu ya msingi na huduma za kisaikolojia kwa makundi yaliyo hatarini na yasiyojiweza, kwa lengo la kuimarisha usawa wa kijamii.

“Tunataka Tanzania yenye usawa wa kiuchumi, mazingira safi, na serikali inayosikia kilio cha kila mwananchi. Hii si ndoto, ni dira ya NLD, na mimi nipo tayari kuiongoza Tanzania mpya yenye matumaini kwa wote,” alisema Mhe. Doyo Hassan Doyo, Mgombea Urais wa NLD.

Katika hatua nyingine, Mhe. Doyo amezungumzia kwa nguvu mpango wa kupunguza matumizi ya mkaa nchini kwa kuhamasisha matumizi ya gesi safi ya kupikia.

Amesema serikali ya NLD itapunguza kodi kwa wawekezaji wanaojihusisha na huduma za gesi, hatua ambayo itafungua milango kwa makampuni kutoa mitungi ya gesi bure kwa Watanzania wote na kupunguza gharama ya gesi ili kila kaya iweze kumudu matumizi ya nishati safi.

“Kama baadhi ya kampuni za simu leo zinatoa laini bure, kesho serikali yangu itahakikisha kila Mtanzania anapata mtungi wa gesi bure. Wajibu wako utakuwa ni kununua gesi pekee, kwa bei nafuu! Hii ndiyo njia ya kisasa ya maendeleo, nishati safi, mazingira salama, maisha bora kwa Watanzania wote,” alisema Mhe. Doyo huku akipigiwa makofi.

Ameongeza kuwa mpango huo utasaidia kupunguza gharama za maisha, kulinda misitu, na kuimarisha uchumi wa kaya, kwani familia nyingi zitaokoa fedha walizokuwa wakitumia kukata miti kwa ajili ya kuni na mkaa.

Pia, serikali yake itapiga marufuku ukataji wa misitu bila kibali maalum na kurasimisha biashara ya mkaa, huku Watanzania wakihimizwa kutumia teknolojia rafiki kwa mazingira.

Mhe. Doyo amesisitiza kuweka mkakati wa kupanda miti milioni 100 katika kipindi cha miaka mitano, ili kurejesha mazingira ya asili, kuhifadhi bioanuai, na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Mhe. Doyo ameomba wananchi wa Kilimanjaro kumpigia kura, huku akiwashauri kuzingatia ahadi zake tano kuu ambazo amezitoa na kuahidi katika mkoa huo. Ahadi hizo ni Kutoa ruzuku kwa watu wenye uhitaji maalum; kuanzisha mfumo maalum wa usimamizi wa haki na maendeleo ya watu wenye ulemavu; kupunguza kodi kwa wawekezaji katika sekta ya gesi safi; kutoa mitungi ya gesi bure kwa Watanzania wote na kupunguza gharama ya gesi ili kumaliza utegemezi wa mkaa na kulinda mazingira; na kujenga taifa lenye usawa wa kiuchumi na fursa sawa kwa kila raia wa Tanzania.

“Ikiwa serikali yangu aitatekeleza haya ndani ya miaka mitano ya utawala wangu, nipo radhi kutochaguliwa tena, na hiyo ndiyo demokrasia. Chagueni Chama cha NLD, chagueni wabunge na madiwani wa NLD, ili tuwatumikie kwa uwajibikaji na uadilifu mkubwa,” alisema Mhe. Doyo.

Kampeni za Mgombea Urais wa NLD zinaelekea mikoa ya Dar es Salaam, Mtwara, na Zanzibar.

Comments

Popular posts from this blog

MWAKIPOSA MWENYEKITI MPYA WA WENYEVITI WA SERIKALI ZA MITAA DAR

Mwenyekiti wa Serikali ya mtaa wa Boko Wilaya ya Kinondoni, Razalous Mwakiposa ameibuka mshindi wa nafasi ya Mwenyekiti wa wenyeviti wa Serikali za mitaa mkoa wa Dar es Salaam kwa kupata kura 24 kati ya 37 zilizopigwa na wajumbe mapema leo hii. Uchaguzi huo umemalizika leo June 20, 2026ambapo  ulikua unahusisha nafasi ya Mwenyekiti na Katibu Mkuu, ambapo Mwenyekiti ameshinda Razalous Mwakiposa huku Katibu Mkuu akiwa ni Peppino Sudi Peppino . Akizungumza wakati wa kutangaza matokeo ya uchaguzi huo, msimamizi wa uchaguzi, Kambi Sinde, amesema kuwa Razalous Mwakiposa ameshinda kwa kupata kura 24 kati ya kura 37 zilizopigwa, huku Katibu Mkuu akishinda kwa kura 20 kati ya kura 37 zilizopigwa. "Uchaguzi umefanyika kwa uwazi na haki, kulikuwa na jumla ya wajumbe 40, lakini watatu walipata udhuru, hivyo, leo waliopiga kura ni wajumbe 37 na matokeo ni kwamba mshindi wa nafasi ya Mwenyekiti amepata kura 24 kati ya kura 37 zilizopigwa, huku Katibu Mkuu akipata kura 20 kati ya kura 37 zilizop...

TIRDO YAVUNJA VIKWAZO VYA UBUNIFU, AFRO HEAL YAGEUZA MIMEA YA ASILI KUWA DAWA ZA KISASA

Na Ayra News.  Mashauri Enock Shushu, kutoka Afro heal Group Limited, amesema malezi ya ubunifu kupitia shirika la Utafiti na Maendeleo ya Viwanda Tanzania (TIRDO) yameiwezeshaa kampuni hiyo kubadili dawa za asili zilizokuwa zikitengenezwa kwa kutumia magome ya miti na kuzigeuza kuwa bidhaa za kisasa zinazokidhi viwango vya ubora na mahitaji utengenezaji soko. Akizungumza katika Maonesho ya Nanenane 2026, Shushu alisema Afro healGroup Limited ni kampuni inayojihusisha na utafiti na utengenezaji wa dawa za binadamu zinazotokana na mimea ya asili, huku TIRDO ikiwa imekuwa nguzo muhimu katika kukuza uwezo wao wa ubunifu na uzalishaji. Alisema kabla ya kujiunga na TIRDO, kampuni hiyo ilikuwa ikitengeneza dawa za asili katika mfumo wa magome, lakini baada ya kupata malezi ya biashara, ushauri wa kitaalamu na uwekezaji wa rasilimali watu kupitia taasisi hiyo, imefanikiwa kuziboresha na kuzalisha bidhaa za kisasa zinazorahisisha matumizi kwa wananchi. Shushu alisema ushirikiano kati ya wa...

VETA KAGERA WABUNI MTEGO KISASA WA KUVUNA SENENE

Ayra Nwestz  Chuo cha Veta mkoa wa Kagera VTC kimebuni mtambo wa kisasa wa kuvuna senene ambao unamuwezesha mvunaji kunapata senene wengi kwa wakati mmoja ambao wanakua salama. Akizungumza na Mtandao wa Matukio Daima, katika maonyesho ya 47 ya biashara ya kimataifa, Mwalimu wa Kagera VTC, Elias Lucas Mayala, amesema chuo hicho kimebuni mtego huo una lengo la kupunguza uharibifu wa mazingira unaotokana na mbinu za jadi za uvunaji. Mayala amesema kuwa mtanbo huo una uwezo wa kubeba kati ya kilo 80 hadi 100 za senene kwa wakati mmoja wakati wa uvunaji.  Aidha, amesema mtego huo una mfumo wa kuchuja senene wanapoingia na kuwatenganisha wadudu wadogo wadogo, ambao wanaweza kutumika kama chakula cha kuku badala ya kutupwa. Ameeleza kuwa tofauti na mbinu za zamani zinazoweza kuharibu miti na mazalia ya senene, mtego huo ni rafiki wa mazingira na umeundwa kwa namna inayorahisisha matumizi yake, ikiwa ni pamoja na uwezo wa kusogezwa kutoka eneo moja kwenda jingine kulingana na mahitaji...