Skip to main content

MD TWANGE AELEZA KUTORIDHISHWA NA KASI YA MKANDARASI WA MRADI WA HALE





Ni ule wa kuboresha kituo cha kufua umeme 

Amuagiza kuongeza kasi ya utekelezaji wa Mradi huo

Na Mwandishi Wetu, Korogwe, Tanga

Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO Bw. Lazaro Twange ameeleza kutoridhishwa na kasi ya mkandarasi anayetekeleza mradi wa maboresho ya Kituo cha Kufua Umeme cha Hale kutokana na kuchelewa kukamilika kwa Mradi huo ulioanza kutekelezwa tangu mwaka 2022.

Bw. Twange ameyasema hayo leo Aprili 22, 2026 wakati wa ziara yake ya ukaguzi katika mradi wa Hale pamoja na mradi wa usafishaji wa bwawa la Mto Pangani iliyopo katika Wilaya ya Korogwe mkoani Tanga ambapo amemtaka mkandarasi wa Mradi wa Hale kuongeza kasi ya utekelezaji wa mradi huo ikiwa ni pamoja na kuongeza wafanyakazi pamoja na muda wa kufanya kazi ili ukamilike kwa wakati.

“Siridhishwi sana na mwenendo wake. Mkandarasi amewahi kuomba nyongeza ya muda mara mbili na nimepata taarifa kuwa yuko kwenye hatua za kuomba nyongeza nyingine ya tatu. Ndio maana nimekuja kuona kuna nini,” amesema Bw. Twange.

Amesema mradi huo una maeneo saba ya utekelezaji ambapo maeneo mawili tayari yamekamilika huku mengine yakiendelea na utekelezaji.

“Nimezungumza na msimamizi wa mradi, mhandisi mshauri pamoja na mkandarasi na nimewaelekeza wakae pamoja kuhakikisha ifikapo mwisho wa mwezi Julai mradi huu uwe umekamilika,” amesema Bw. Twange

Aidha, kuhusu mradi wa usafishaji wa bwawa la Pangani, Bw. Twange amesema matarajio ya TANESCO ni kuhakikisha kazi hiyo inakamilika ndani ya muda uliopangwa ili kuepusha changamoto zinazoweza kujitokeza wakati wa msimu wa mvua.

“Matarajio yetu ni kutoupitiliza mwaka mmoja ili tumalize kabla ya msimu unaokuja wa mvua,” ameongeza.

Katika hatua nyingine, Bw. Twange amesema TANESCO kwa sasa inaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo ya umeme nchini yenye thamani ya zaidi ya shilingi trilioni 13.4.

Kwa upande wake, Meneja wa Mradi wa Mradi wa Hale Mha. Kulwa Byemelo amesema maagizo yaliyotolewa na Mkurugenzi Mtendaji yatatekelezwa ili kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati.

“Mradi huu utakapokamilika utaimarisha upatikanaji wa umeme katika wilaya mbalimbali zinazochukua umeme kutoka kituo cha Hale pamoja na wilaya za Handeni, Muheza na Korogwe,” amesema Byemelo.

Ziara hii ni moja ya mikakati ya kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya umeme pamoja na kubaini changamoto zinazojitokeza na kuhakikisha zinatatuliwa kwa wakati na miradi ina kamilika ili watanzania waweze kuendelea kufurahia upatikanaji wa umeme wa uhakika.

Comments

Popular posts from this blog

MWAKIPOSA MWENYEKITI MPYA WA WENYEVITI WA SERIKALI ZA MITAA DAR

Mwenyekiti wa Serikali ya mtaa wa Boko Wilaya ya Kinondoni, Razalous Mwakiposa ameibuka mshindi wa nafasi ya Mwenyekiti wa wenyeviti wa Serikali za mitaa mkoa wa Dar es Salaam kwa kupata kura 24 kati ya 37 zilizopigwa na wajumbe mapema leo hii. Uchaguzi huo umemalizika leo June 20, 2026ambapo  ulikua unahusisha nafasi ya Mwenyekiti na Katibu Mkuu, ambapo Mwenyekiti ameshinda Razalous Mwakiposa huku Katibu Mkuu akiwa ni Peppino Sudi Peppino . Akizungumza wakati wa kutangaza matokeo ya uchaguzi huo, msimamizi wa uchaguzi, Kambi Sinde, amesema kuwa Razalous Mwakiposa ameshinda kwa kupata kura 24 kati ya kura 37 zilizopigwa, huku Katibu Mkuu akishinda kwa kura 20 kati ya kura 37 zilizopigwa. "Uchaguzi umefanyika kwa uwazi na haki, kulikuwa na jumla ya wajumbe 40, lakini watatu walipata udhuru, hivyo, leo waliopiga kura ni wajumbe 37 na matokeo ni kwamba mshindi wa nafasi ya Mwenyekiti amepata kura 24 kati ya kura 37 zilizopigwa, huku Katibu Mkuu akipata kura 20 kati ya kura 37 zilizop...

TIRDO YAVUNJA VIKWAZO VYA UBUNIFU, AFRO HEAL YAGEUZA MIMEA YA ASILI KUWA DAWA ZA KISASA

Na Ayra News.  Mashauri Enock Shushu, kutoka Afro heal Group Limited, amesema malezi ya ubunifu kupitia shirika la Utafiti na Maendeleo ya Viwanda Tanzania (TIRDO) yameiwezeshaa kampuni hiyo kubadili dawa za asili zilizokuwa zikitengenezwa kwa kutumia magome ya miti na kuzigeuza kuwa bidhaa za kisasa zinazokidhi viwango vya ubora na mahitaji utengenezaji soko. Akizungumza katika Maonesho ya Nanenane 2026, Shushu alisema Afro healGroup Limited ni kampuni inayojihusisha na utafiti na utengenezaji wa dawa za binadamu zinazotokana na mimea ya asili, huku TIRDO ikiwa imekuwa nguzo muhimu katika kukuza uwezo wao wa ubunifu na uzalishaji. Alisema kabla ya kujiunga na TIRDO, kampuni hiyo ilikuwa ikitengeneza dawa za asili katika mfumo wa magome, lakini baada ya kupata malezi ya biashara, ushauri wa kitaalamu na uwekezaji wa rasilimali watu kupitia taasisi hiyo, imefanikiwa kuziboresha na kuzalisha bidhaa za kisasa zinazorahisisha matumizi kwa wananchi. Shushu alisema ushirikiano kati ya wa...

VETA KAGERA WABUNI MTEGO KISASA WA KUVUNA SENENE

Ayra Nwestz  Chuo cha Veta mkoa wa Kagera VTC kimebuni mtambo wa kisasa wa kuvuna senene ambao unamuwezesha mvunaji kunapata senene wengi kwa wakati mmoja ambao wanakua salama. Akizungumza na Mtandao wa Matukio Daima, katika maonyesho ya 47 ya biashara ya kimataifa, Mwalimu wa Kagera VTC, Elias Lucas Mayala, amesema chuo hicho kimebuni mtego huo una lengo la kupunguza uharibifu wa mazingira unaotokana na mbinu za jadi za uvunaji. Mayala amesema kuwa mtanbo huo una uwezo wa kubeba kati ya kilo 80 hadi 100 za senene kwa wakati mmoja wakati wa uvunaji.  Aidha, amesema mtego huo una mfumo wa kuchuja senene wanapoingia na kuwatenganisha wadudu wadogo wadogo, ambao wanaweza kutumika kama chakula cha kuku badala ya kutupwa. Ameeleza kuwa tofauti na mbinu za zamani zinazoweza kuharibu miti na mazalia ya senene, mtego huo ni rafiki wa mazingira na umeundwa kwa namna inayorahisisha matumizi yake, ikiwa ni pamoja na uwezo wa kusogezwa kutoka eneo moja kwenda jingine kulingana na mahitaji...