Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, ameipongeza kampuni ya Nida kwa kuzalisha bidhaa zenye ubora unaoendana na soko, huku akisisitiza kuwa wanatambua kazi kubwa inayofanywa na kampuni hiyo katika kuunga mkono juhudi za Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dkt Samia.
Waziri Kapinga ametembelea banda la Kiwanda cha NIDA katika Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba) yanayoendelea jijini Dar es Salaam ambapo amesema ameridhishwa na ubora unaozalisha katika bidhaa.
Akizungumza na waandishi wa habari, Meneja wa Mahusiano wa NIDA, Mohamed Honelo, amesema kampuni hiyo, imejenga mnyororo kamili wa uzalishaji unaoanzia kwa kuwawezesha wakulima wa pamba, kununua mazao yao, kuyasindika kuwa nyuzi na vitambaa katika kiwanda chake kilichopo Mbeya, kisha kuvipeleka NIDA Textile Mills kwa ajili ya uchapishaji kabla ya kuviuza kupitia maduka yake.
Aidha, kampuni hiyo imechangia kwa kiasi kikubwa katika kutatua changamoto ya ajira kwa kutoa ajira za moja kwa moja kati ya 1,500 na 2,000, pamoja na ajira za muda kulingana na mahitaji ya uzalishaji.
Sambamba na hilo, amesema mfumo huo unaendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050 inayolenga kuongeza viwanda nchini, kuzalisha ajira, kukuza biashara na kuongeza mchango wa sekta ya viwanda katika uchumi wa Taifa.
Hata hivyo, amesema kuwa bidhaa za kampuni hiyo, zikiwemo kanga, vitenge, mashuka na bidhaa nyingine zinazotokana na pamba, zinapatikana katika maduka ya NIDA na NIDA Textile Mills, huku akiwakaribisha wananchi kuzinunua na kuunga mkono bidhaa zinazozalishwa nchini.
Aidha, Honelo aliiomba Serikali kuweka utaratibu utakaowezesha sehemu kubwa ya pamba inayozalishwa nchini kubaki kwa matumizi ya viwanda vya ndani badala ya kuuzwa nje kama malighafi.
“Tunaiomba Serikali iweke akiba ya pamba kwa ajili ya viwanda vya ndani. Ni kweli hatuwezi kununua pamba yote kwa wakati mmoja, lakini kiasi kinachobaki kihifadhiwe ili baadaye viwanda vya ndani viweze kukinunua badala ya kulazimika kuagiza au kununua pamba hiyo hiyo kwa gharama kubwa kutoka nje,”amesema Honelo.
Ameongeza kuwa, pia gharama kubwa za uzalishaji zinapunguza uwezo wa viwanda vya ndani kushindana na bidhaa kutoka nje, huku wazalishaji wa nchi nyingine wakinufaika na gharama ndogo za uzalishaji zinazowaruhusu kuuza bidhaa kwa bei nafuu zaidi.
"Naipongeza Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuendelea kuhamasisha maendeleo ya sekta ya viwanda, akisema hatua hiyo itaongeza ajira, kukuza uchumi na kuifanya Tanzania kuwa taifa lenye msingi imara wa viwanda"amesema




Comments
Post a Comment