Ayra news
Jitihada za Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) kuonesha fursa za uwekezaji na miradi yake ya kimkakati katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba), zimezaa matunda baada ya taasisi hiyo kutwaa tuzo ya mshindi wa pili katika kipengele cha Banda Bora upande wa Sekta ya Miliki na Real Estate.
Tuzo hiyo ilikabidhiwa wakati wa sherehe za kufunga maonesho hayo zilizofanyika Julai 13, 2026, na kupokewa na Mkurugenzi wa Huduma Saidizi wa TBA, Amina Lumuli, kwa niaba ya Mtendaji Mkuu wa taasisi hiyo, Arch. Daud W. Kondoro.
Akizungumza baada ya kupokea tuzo hiyo, Bi. Lumuli alisema mafanikio hayo yanadhihirisha namna TBA ilivyoweza kutumia maonesho hayo kuwasogezea wananchi huduma, kutoa elimu kuhusu majukumu yake na kufungua milango ya fursa kwa wawekezaji kupitia miradi ya ubia kati ya sekta ya umma na binafsi (PPP).
Alisema banda la TBA lilikuwa kivutio kwa wageni wengi waliotembelea maonesho hayo kutokana na maelezo kuhusu miradi mbalimbali inayotekelezwa nchini, ikiwemo ujenzi wa nyumba za gharama nafuu, majengo ya taasisi za umma na kazi za ukarabati pamoja na uboreshaji wa miundombinu ya michezo, ukiwemo Uwanja wa Benjamin Mkapa.
Kwa mujibu wa Bi. Lumuli, mwitikio wa wananchi na wadau umeongeza imani kwa TBA na kuthibitisha kuwa taasisi hiyo inaendelea kuwa miongoni mwa vinara wa utekelezaji wa miradi ya ujenzi yenye viwango vya kitaalamu na mchango mkubwa katika maendeleo ya Taifa.
Alitoa wito kwa sekta binafsi na wawekezaji kutumia fursa zilizopo kushirikiana na TBA katika utekelezaji wa miradi ya ubia, akisema ushirikiano huo utasaidia kuongeza kasi ya maendeleo ya miundombinu na kuboresha huduma kwa wananchi.
Sherehe za kufunga Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Sabasaba ziliongozwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, ambapo taasisi mbalimbali zilizofanya vizuri zilitunukiwa tuzo kwa kutambua ubunifu na mchango wao katika utoaji wa huduma kwa umma.


Comments
Post a Comment