Na Ayra Newstz
Viongozi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam wametoa wito kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kuchangamkia mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri, wakieleza kuwa fedha hizo zimeendelea kubadilisha maisha ya wananchi kwa kuwawezesha kuanzisha na kukuza biashara pamoja na viwanda vidogo.
Wito huo umetolewa walipotembelea Banda la Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), ambapo pia walipongeza maandalizi ya maonesho hayo na ubora wa bidhaa zinazozalishwa na wajasiriamali wa Tanzania.
Akizungumza katika maonesho hayo, kiongozi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam amesema anaungana na Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, kuwapongeza waandaaji wa maonesho hayo kwa kufanikisha tukio hilo ambalo limeendelea kuwa jukwaa muhimu la kukuza biashara, uwekezaji na ubunifu wa wazalishaji wa ndani.
Amesema ubora wa bidhaa zinazozalishwa na wajasiriamali wa Tanzania umeongezeka kwa kiwango kikubwa na sasa zinaweza kushindana katika masoko mbalimbali kutokana na maboresho ya viwango vya uzalishaji.
Akitolea mfano bidhaa za ngozi na viatu vinavyozalishwa nchini, amesema vina ubora unaoweza kushindana na bidhaa nyingine katika maduka makubwa na masoko ya ndani na nje ya nchi.
Kuhusu mikopo ya asilimia 10, amesema utekelezaji wake umeleta mafanikio makubwa kwa vikundi mbalimbali ambavyo vimefanikiwa kuanzisha viwanda vidogo na kupanua shughuli zao za uzalishaji baada ya kunufaika na fedha hizo.
Amesema baadhi ya vikundi vimepokea mikopo inayofikia zaidi ya Sh milioni 80 na vingine zaidi ya Sh milioni 30, hali ambayo imechangia kukuza uchumi wa wananchi na kuongeza ajira.
"Tumeshuhudia vikundi vimeanzisha mpaka viwanda vidogo vidogo baada ya kupata mikopo hii. Hii inaonyesha fedha hizi zina matokeo chanya na zinaendelea kubadilisha maisha ya wananchi," amesema.
Ameongeza kuwa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam itaendelea kutenga na kutoa mikopo hiyo kupitia maamuzi ya Baraza la Madiwani ili kuhakikisha makundi yanayolengwa yanaendelea kunufaika.
Aidha, amesema halmashauri imeimarisha mfumo wa usimamizi wa mikopo hiyo kwa kushirikiana na taasisi za kifedha ili kuhakikisha fedha zinarejeshwa kwa wakati na kuwafikia wanufaika wengi zaidi.
Amesema katika maonesho hayo pia kuna dawati maalumu la utoaji elimu kwa wananchi kuhusu utaratibu wa kuomba, kupata na kurejesha mikopo hiyo ili kuongeza uelewa na ushiriki wa wananchi.
Kwa mujibu wa kiongozi huyo, Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam imetenga zaidi ya Sh bilioni 22 kwa ajili ya mikopo ya asilimia 10 kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, huku ikiendelea kutekeleza maelekezo ya Serikali ya kuboresha mazingira ya biashara kwa kutenga fedha za ujenzi wa miundombinu ya wajasiriamali
Amesema fedha hizo zitaelekezwa katika ujenzi wa maeneo ya uzalishaji, viwanda vidogo na masoko ya kisasa yatakayowawezesha wajasiriamali kuongeza thamani ya bidhaa zao na kupata masoko yenye uhakika
Amewataka wananchi kutembelea Banda la Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam katika Maonesho ya Sabasaba ili kupata elimu kuhusu fursa mbalimbali zinazotolewa na halmashauri pamoja na kujionea mafanikio ya vikundi vilivyonufaika na mikopo hiyo.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji, Elihuruma Mabelya amesema Jiji limetumia Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) kujifunza mbinu zitakazosaidia kuboresha utoaji wa huduma za ardhi, kupunguza migogoro ya umiliki na kurahisisha upatikanaji wa hati kwa wananchi.
Amesema kuwa, kupitia ziara hiyo imewapa viongozi nafasi ya kujionea huduma zinazotolewa na Wizara ya Ardhi pamoja na kazi inayofanywa na watumishi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam katika kuwahudumia wananchi.
Mabelya amesema kupitia banda hilo wamejifunza umuhimu wa kuwa na kituo cha pamoja cha utoaji wa huduma za ardhi kitakachorahisisha upatikanaji wa hati, leseni za makazi, ulipaji wa kodi ya ardhi pamoja na huduma nyingine zinazohusu sekta hiyo.
"Kituo cha pamoja cha huduma za ardhi kinaweza kutusaidia kupunguza malalamiko ya wananchi na changamoto wanazokutana nazo katika utoaji wa hati, leseni za makazi na huduma nyingine za ardhi," amesema.
Amesema Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam itatumia mafunzo yaliyopatikana katika maonesho hayo kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi na kuongeza ufanisi katika kushughulikia masuala ya ardhi.
Naye, Meya wa jiji la Dar es Salaam Nurdin Bilal amesema mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu imeanza kuonesha matokeo baada ya baadhi ya wanufaika kutumia fedha hizo kuanzisha viwanda vidogo na kupanua uzalishaji wa bidhaa.
Bilal amesema baadhi ya vikundi vilivyonufaika na mikopo hiyo vimeweza kupiga hatua kubwa kiuchumi, huku vingine vikifikia hatua ya kuanzisha viwanda vidogo baada ya kupata fedha za kuwawezesha kuongeza uzalishaji.
"Tumeshuhudia kuna vikundi pale vimeanzisha mpaka viwanda vidogo vidogo na vimepata zaidi ya Sh milioni 80 za kuendelea. Wengine wamepata milioni 30 na huu ni mfano tu, wapo wengi wa aina hiyo,"aamesema.
Hata hivyo, amesema mafanikio hayo yanaonesha kuwa mikopo hiyo si suala la maneno pekee bali ni chachu ya kuwawezesha wananchi kujenga shughuli zao za kiuchumi.








Comments
Post a Comment