Skip to main content

MTENDAJI MKUU WMA AHAMASISHA WANANCHI KUTUMIA MIZANI ILIYOHAKIKIWA


Na WMA - DODOMA

WAKALA wa Vipimo  (WMA) umewataka wafanyabiashara na wananchi kuacha mara moja matumizi ya vipimo visivyo rasmi, ikiwemo ndoo, mafungu, visado na makopo, katika uuzaji wa mazao ya kilimo na mifugo na badala yake kutumia mizani iliyohakikiwa kwa mujibu wa sheria.

Wito huo umetolewa na Afisa Mtendaji Mkuu wa WMA, Alban Kihula, leo Agosti 8, 2026 wakati akizungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya 33 ya Kitaifa ya Siku ya Wakulima Nane Nane, yaliyokuwa yakifanyika katika Viwanja vya Dkt. John Samwel Malecela, jijini Dodoma.


Kihula amesema matumizi ya vipimo visivyo rasmi yanaweza kusababisha kutokuwepo kwa usawa katika biashara na kuwaathiri wananchi kwa kuwafanya wasipate thamani halisi ya bidhaa wanazonunua au kuuza.

Amesema WMA imeendelea kutoa elimu kwa wananchi, wakulima, wafugaji na wafanyabiashara kuhusu matakwa ya Sheria ya Vipimo, Sura ya 340, ikiwemo namna ya kutambua vipimo vilivyohakikiwa na uwekaji wa alama sahihi kwenye bidhaa zilizofungashwa.

“Ili kuwa na soko lenye haki na kuongeza tija kuelekea Dira ya 2050, hakuna soko linaloweza kuwa la haki bila matumizi ya vipimo vilivyohakikiwa kwa mujibu wa sheria,” amesema Kihula.


Akizungumzia sekta ya kilimo, Kihula amewataka wakulima kuzingatia matumizi ya vipimo sahihi katika hatua zote za uzalishaji na biashara, kuanzia uandaaji wa mashamba hadi uvunaji, uhifadhi na uuzaji wa mazao.

Amesema matumizi ya vipimo sahihi katika kujua ukubwa wa eneo la shamba yanaweza kusaidia wakulima kupanga uzalishaji kwa usahihi badala ya kutegemea makadirio.

Aidha, amewataka kuhakikisha mazao yanapimwa kwa mizani iliyohakikiwa wakati wa kuuza ili mkulima aweze kupata thamani halisi ya bidhaa zake.


Kwa upande wa wafugaji, Kihula amewataka kuacha kuuza mifugo kwa kutegemea makadirio ya macho na badala yake kutumia mizani sahihi katika kubaini uzito wa mifugo kama vile ng'ombe, mbuzi, kondoo na kuku.

Amesema utaratibu huo unapaswa pia kuzingatiwa katika uuzaji wa bidhaa zinazotokana na mifugo, ikiwemo nyama na maziwa, ili kuhakikisha mnunuzi na muuzaji wanapata thamani inayolingana na kiasi cha bidhaa kinachouzwa.

Wakati huohuo, Kihula amewapongeza wavuvi kwa kuendelea kuonesha mfano mzuri katika matumizi ya vipimo na kuwataka kuendeleza utaratibu huo.


Amesema matumizi ya vipimo sahihi katika shughuli za uvuvi ni muhimu katika kuhakikisha biashara inafanyika kwa uwazi na kwa kuzingatia thamani halisi ya bidhaa.

Kihula amewataka wananchi kuwa mstari wa mbele kukataa kuhudumiwa kwa vipimo visivyo rasmi wanaponunua bidhaa kama vile viazi, bamia, vitunguu na nyanya, badala yake kusisitiza bidhaa hizo zipimwe kwa mizani iliyohakikiwa.

“Wananchi wasikubali kununua bidhaa kwa mafungu, visado au vipimo vingine visivyo rasmi. Wanapaswa kusisitiza kupimiwa kwa mizani iliyohakikiwa ili kuhakikisha wanapata kiasi sahihi cha bidhaa wanacholipia,” amesema.


Aidha, amewataka wananchi kutoa taarifa kwa WMA wanapobaini matumizi ya vipimo visivyo halali katika maeneo yao ili hatua stahiki za kisheria ziweze kuchukuliwa.

Amesema ushirikiano wa wananchi, wafanyabiashara na taasisi za Serikali ni muhimu katika kujenga soko lenye haki, uwazi na linalozingatia matumizi ya vipimo sahihi kwa mujibu wa sheria.

Amesisitiza kuwa matumizi ya vipimo vilivyohakikiwa si suala la wafanyabiashara pekee, bali ni jambo linalomhusu kila mwananchi katika kuhakikisha anapata thamani halisi ya fedha anayolipa au mapato anayopata kutokana na bidhaa anazouza.

Comments

Popular posts from this blog

MWAKIPOSA MWENYEKITI MPYA WA WENYEVITI WA SERIKALI ZA MITAA DAR

Mwenyekiti wa Serikali ya mtaa wa Boko Wilaya ya Kinondoni, Razalous Mwakiposa ameibuka mshindi wa nafasi ya Mwenyekiti wa wenyeviti wa Serikali za mitaa mkoa wa Dar es Salaam kwa kupata kura 24 kati ya 37 zilizopigwa na wajumbe mapema leo hii. Uchaguzi huo umemalizika leo June 20, 2026ambapo  ulikua unahusisha nafasi ya Mwenyekiti na Katibu Mkuu, ambapo Mwenyekiti ameshinda Razalous Mwakiposa huku Katibu Mkuu akiwa ni Peppino Sudi Peppino . Akizungumza wakati wa kutangaza matokeo ya uchaguzi huo, msimamizi wa uchaguzi, Kambi Sinde, amesema kuwa Razalous Mwakiposa ameshinda kwa kupata kura 24 kati ya kura 37 zilizopigwa, huku Katibu Mkuu akishinda kwa kura 20 kati ya kura 37 zilizopigwa. "Uchaguzi umefanyika kwa uwazi na haki, kulikuwa na jumla ya wajumbe 40, lakini watatu walipata udhuru, hivyo, leo waliopiga kura ni wajumbe 37 na matokeo ni kwamba mshindi wa nafasi ya Mwenyekiti amepata kura 24 kati ya kura 37 zilizopigwa, huku Katibu Mkuu akipata kura 20 kati ya kura 37 zilizop...

TIRDO YAVUNJA VIKWAZO VYA UBUNIFU, AFRO HEAL YAGEUZA MIMEA YA ASILI KUWA DAWA ZA KISASA

Na Ayra News.  Mashauri Enock Shushu, kutoka Afro heal Group Limited, amesema malezi ya ubunifu kupitia shirika la Utafiti na Maendeleo ya Viwanda Tanzania (TIRDO) yameiwezeshaa kampuni hiyo kubadili dawa za asili zilizokuwa zikitengenezwa kwa kutumia magome ya miti na kuzigeuza kuwa bidhaa za kisasa zinazokidhi viwango vya ubora na mahitaji utengenezaji soko. Akizungumza katika Maonesho ya Nanenane 2026, Shushu alisema Afro healGroup Limited ni kampuni inayojihusisha na utafiti na utengenezaji wa dawa za binadamu zinazotokana na mimea ya asili, huku TIRDO ikiwa imekuwa nguzo muhimu katika kukuza uwezo wao wa ubunifu na uzalishaji. Alisema kabla ya kujiunga na TIRDO, kampuni hiyo ilikuwa ikitengeneza dawa za asili katika mfumo wa magome, lakini baada ya kupata malezi ya biashara, ushauri wa kitaalamu na uwekezaji wa rasilimali watu kupitia taasisi hiyo, imefanikiwa kuziboresha na kuzalisha bidhaa za kisasa zinazorahisisha matumizi kwa wananchi. Shushu alisema ushirikiano kati ya wa...

VETA KAGERA WABUNI MTEGO KISASA WA KUVUNA SENENE

Ayra Nwestz  Chuo cha Veta mkoa wa Kagera VTC kimebuni mtambo wa kisasa wa kuvuna senene ambao unamuwezesha mvunaji kunapata senene wengi kwa wakati mmoja ambao wanakua salama. Akizungumza na Mtandao wa Matukio Daima, katika maonyesho ya 47 ya biashara ya kimataifa, Mwalimu wa Kagera VTC, Elias Lucas Mayala, amesema chuo hicho kimebuni mtego huo una lengo la kupunguza uharibifu wa mazingira unaotokana na mbinu za jadi za uvunaji. Mayala amesema kuwa mtanbo huo una uwezo wa kubeba kati ya kilo 80 hadi 100 za senene kwa wakati mmoja wakati wa uvunaji.  Aidha, amesema mtego huo una mfumo wa kuchuja senene wanapoingia na kuwatenganisha wadudu wadogo wadogo, ambao wanaweza kutumika kama chakula cha kuku badala ya kutupwa. Ameeleza kuwa tofauti na mbinu za zamani zinazoweza kuharibu miti na mazalia ya senene, mtego huo ni rafiki wa mazingira na umeundwa kwa namna inayorahisisha matumizi yake, ikiwa ni pamoja na uwezo wa kusogezwa kutoka eneo moja kwenda jingine kulingana na mahitaji...