Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
WAKALA wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) umewapa elimu wafanyabiashara na wachongaji wa vinyago katika eneo la Mwenge jijini Dar es Salaam kuhusu sheria, kanuni na taratibu za uvunaji, usafirishaji na biashara ya mazao ya misitu, ikiwemo namna ya kusafirisha bidhaa hizo nje ya nchi.
Akizungumza wakati wa zoezi hilo jana, Agosti 12, 2026, Mhifadhi wa Misitu wa TFS Wilaya za Kinondoni na Ubungo, Dotto Ndumbikwa, alisema hatua hiyo inalenga kuwawezesha wafanyabiashara kuelewa taratibu zinazotakiwa, kufanya biashara zao kwa ufanisi na kuepuka usumbufu unaoweza kujitokeza kutokana na kutofuata sheria.
Ndumbikwa alisema TFS imeambatana na wahifadhi kutoka Kanda ya Mashariki, wakiwemo wanaosimamia shughuli za misitu katika eneo la Uwanja wa Ndege, kwa lengo la kusikiliza changamoto za wafanyabiashara na kuzitafutia ufumbuzi. “Tunapokaa kuwasikiliza na kuwapa elimu, inawasaidia wao kuendelea na biashara zao vizuri bila kupata matatizo,” alisema.
Aliwataka wafanyabiashara wa mazao ya misitu kufika katika ofisi husika za Serikali kabla ya kuanza biashara ili kupata elimu kuhusu taratibu, vibali na tozo zinazohitajika. Pia aliwataka kuwa makini wakati wa ukaguzi wa bidhaa zao, hususan viwanja vya ndege, kwa kuhakikisha afisa anayefanya ukaguzi anajitambulisha na kuonyesha kitambulisho cha kazi.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Wasanii Wachongaji Tanzania (CHAWASAWATA), Sebastian Daniel Mbebe, alisema elimu hiyo imewasaidia kuelewa sheria na taratibu ambazo awali zilikuwa chanzo cha changamoto, akisema wachongaji nao wamebaini baadhi ya maeneo ambayo hawakuwa wakifuata ipasavyo, ikiwemo kuwa na vibali vinavyotakiwa. “Hata sisi upande wetu kama uchongaji tulikuwa na makosa. Kuna vibali vingi tulikuwa hatuvitekelezi kwa mujibu wa sheria inavyotakiwa, lakini leo tumepata elimu na tumejua tunachotakiwa kufanya,” alisema.
Hata hivyo, Mbebe alisema bado kuna changamoto ya tozo wanazoziona kuwa kubwa, hasa kwa vinyago vya twiga, faru, simba na tembo ambavyo vinaweza kuwa na uzito mkubwa licha ya kuwa tayari ni bidhaa za sanaa. Alisema hali hiyo inaweza kuongeza gharama kwa wateja wanaosafirisha bidhaa hizo kupitia viwanja vya ndege, huku akieleza kuwa wataendelea kufuata taratibu na kulipia vibali vinavyohitajika wakati wakisubiri hatua zaidi kuhusu mapitio ya tozo hizo.
Naye mdau wa mazao ya misitu, Mwanne Mashugu, aliishukuru TFS kwa kuwafikia katika eneo lao la biashara na kuwapa elimu kuhusu taratibu kuanzia kupata mazao hadi kuyafikisha madukani, pamoja na namna ya kulipia tozo na kupata vibali vya usafirishaji. “Kwa elimu tuliyopewa tutaweza kuwaelimisha wateja wetu na kuwasaidia kufanikiwa kupita na mizigo yao salama bila mizigo yao kubaki pale uwanja wa ndege,” alisema.
TFS imeendelea kuwasisitiza wafanyabiashara na wadau wa mazao ya misitu kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa, huku ikiwataka kupata elimu na vibali kutoka katika ofisi husika za Serikali kabla ya kuanza biashara au kusafirisha bidhaa hizo nje ya nchi.


Comments
Post a Comment