Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imesema mvua za msimu wa Vuli za Oktoba hadi Desemba 2026 zinatarajiwa kuwa za wastani hadi juu ya wastani katika maeneo mbalimbali nchini, huku uwepo wa hali ya El Niño ukitajwa kuwa miongoni mwa sababu zinazoweza kuchangia vipindi vya mvua kubwa katika baadhi ya maeneo.
Akizungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam wakati akitoa mwelekeo wa mvua hizo, Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dkt. Ladislaus Chang’a, amesema mvua hizo zinatarajiwa kuanza katika wiki ya kwanza na ya pili ya Oktoba katika baadhi ya maeneo.
Amesema katika mikoa ya Arusha na Manyara, mvua zinatarajiwa kuwa za wastani hadi juu ya wastani, huku hali kama hiyo ikitarajiwa pia katika ukanda wa Kaskazini unaojumuisha Tanga, Dar es Salaam, kaskazini mwa Morogoro pamoja na visiwa vya Mafia na Pemba.
TMA imesema uwepo wa El Niño unaweza kuchangia kuongezeka kwa vipindi vya mvua kubwa, hali ambayo inaweza kusababisha mafuriko na athari katika miundombinu, kilimo, usafiri na shughuli nyingine za kijamii na kiuchumi.
El Niño ni hali ya mabadiliko ya mfumo wa joto la bahari katika eneo la Pasifiki ya ikweta, ambayo huathiri mifumo ya hewa duniani na inaweza kusababisha mabadiliko ya mvua na joto katika maeneo mbalimbali. Kwa Tanzania, hali hiyo inaweza kuhusishwa na ongezeko la mvua katika baadhi ya maeneo, ingawa athari zake hutofautiana kulingana na eneo na kipindi.
Kutokana na hali hiyo, TMA imewataka wananchi kufuatilia taarifa rasmi za hali ya hewa na kuchukua tahadhari mapema, hasa katika maeneo yanayoweza kukumbwa na mvua kubwa na mafuriko.
TMA pia imesema hali hiyo inaweza kuchangia kuanza mapema kwa mvua za msimu wa Novemba hadi Aprili katika baadhi ya maeneo yanayopata msimu huo.
Katika sekta ya kilimo, TMA imesema kuongezeka kwa unyevunyevu wa udongo na uwezekano wa mafuriko kunaweza kuathiri ukuaji wa mazao na shughuli za kilimo, huku mazingira yenye unyevunyevu yakitarajiwa pia kuchochea kuibuka kwa baadhi ya magonjwa ya mimea.
Wakulima wametakiwa kuandaa mashamba, kupanda na kupalilia kwa wakati, kutumia pembejeo zinazofaa na kuzingatia ushauri wa wataalamu.
Kwa wafugaji, TMA imeshauri kuandaa malisho na kuhifadhi maji ya kutosha kwa matumizi ya mifugo, huku wakitakiwa kufuatilia taarifa za hali ya hewa na kupata ushauri kutoka kwa maafisa mifugo.
Wavuvi na wakulima wa mwani nao wametakiwa kufuatilia taarifa za hali ya hewa na hali ya bahari kabla ya kufanya shughuli zao.
TMA imeonya kuwa mvua kubwa zinazoweza kuambatana na vipindi vya El Niño zinaweza pia kuathiri barabara, madaraja na miundombinu mingine ya usafiri kutokana na mafuriko na mmomonyoko wa udongo.
Mamlaka za serikali za mitaa zimetakiwa kujiandaa kwa kuboresha mifumo ya mifereji ya maji, kuondoa vizuizi kwenye njia za maji na kutoa elimu kwa wananchi kuhusu tahadhari za kuchukua wakati wa mvua kubwa.
Katika sekta ya afya, TMA imeonya kuhusu uwezekano wa kuongezeka kwa magonjwa kutokana na maji kutuama, kuathirika kwa mifumo ya maji taka na changamoto katika usafi wa mazingira.
Aidha, TMA imevitaka vyombo vya habari kuendelea kutumia taarifa rasmi za hali ya hewa katika kuhabarisha na kuelimisha jamii kuhusu mabadiliko ya hali ya hewa na tahadhari zinazopaswa kuchukuliwa.
Mamlaka hiyo imesema imeendelea kujenga uwezo wa kutoa utabiri wa hali ya hewa hadi ngazi ya wilaya, hatua inayolenga kuwawezesha wananchi, wakulima, wafugaji, wafanyabiashara na serikali za mitaa kupanga shughuli zao kwa kuzingatia taarifa za hali ya hewa.
TMA imewataka wananchi kuendelea kufuatilia taarifa za kila siku, angalizo na tahadhari zitakazotolewa, ikisisitiza kuwa kuchukua hatua mapema ni muhimu katika kupunguza madhara yanayoweza kusababishwa na mvua kubwa.



Comments
Post a Comment